NI utoto wa mjini tu na kukomoana. Wakala wa
kipa namba moja wa Manchester United, David de Gea, Jorge Mendes
inadaiwa kuwa analazimisha dili la kumuuza kipa huyo mahiri kwenda Real
Madrid ya Hispania.
Imedaiwa kuwa Mendes amekerwa na
kitendo cha Manchester United kumbabaisha mteja wake mwingine, Radamel
Falcao, ambaye hana maisha mazuri Old Trafford na anatumia hasira hizo
kutaka kulazimisha kumuuza De Gea kwenda Santiago Bernabeu.
Mendes amelipeleka jina la De
Gea katika meza ya mabosi wa Real Madrid kwa ajili ya kuangalia
uwezekano wa kumhamisha mteja wake huyo, ambaye anahusudiwa na mabosi wa
timu hiyo wanaomuona kama mbadala wa muda mrefu wa kipa wao wa sasa,
Iker Casillas.
Na Madrid wako tayari kutoa dau
la Pauni 50 milioni na kuvunja rekodi ya uhamisho kwa makipa ambayo
mpaka sasa inashikiliwa na kipa wa Juventus, Gianluigi Buffon ambaye
alihamishwa kwa dau la Euro 51 milioni kutoka Parma mwaka 2001.
Mendes anajulikana kwa
kuwamiliki wachezaji wenye majina makubwa katika soka kwa sasa kama
Falcao, De Gea, Angel Di Maria, Cristiano Ronaldo na wengineo. Uhusiano
wake na Manchester United umekuwa imara tangu enzi za Sir Alex Ferguson
ambaye amewahi kumuelezea Mendes kama ‘Wakala bora aliyekuwa akifanya
naye kazi.”
Lakini uhusiano huo unaonekana
kuvunjika baada ya kocha wa Man United, Louis van Gaal kumshambulia
Mendes wiki iliyopita kwa maelezo yake aliyotoa kuhusu Falcao baada ya
nyota huyo wa Colombia kupigwa benchi katika pambano dhidi ya
Southampton.
Kwa sasa De Gea anachukuliwa
kama mmoja kati ya makipa bora duniani na mkataba wake unatazamiwa
kumalizika mwishoni mwa msimu ujao. Man United inataka kumpa mkataba
wenye thamani ya Pauni 200,000 kwa wiki lakini inadaiwa kuwa De Gea
anavutika na uhamisho wa kurudi kwao Hispania.
De Gea ametwaa taji moja na
Manchester United ambalo ni ubingwa wa Ligi Kuu England tangu alipohamia
Old Trafford kutoka Atletico Madrid kwa dau la Pauni 17 milioni mwaka
2011.
Kama watamuuza De Gea Man United
hawatapata pigo kubwa kwani wamefanikiwa kuinasa saini ya kipa wa
zamani wa Barcelona, Victor Valdes ambaye aliwahi kucheza chini ya Van
Gaal akiwa Barcelona 2002 mpaka 2003.
0 comments: