Powered by Blogger.

Monday 16 February 2015

Siri ya wanaume kupenda kuvaa suruali nyeusi

Posted by Unknown at 23:41 0 Comments


 
Nimesimama Kituo cha Daladala Mbezi Mwisho, saa moja asubuhi kusubiri usafiri wa kuelekea kazini. Watu ni wengi, kila mmoja yuko makini kufuatilia mabasi yanayoingia kituoni hapo.
Mara basi la Mbezi- Gongo la Mboto linawasili, kabla hata halijasimama kushusha abiria, watu wanalikimbilia, wanajazana mlangoni, wengine wanaingia ndani kupitia kwenye madirisha.
Mimi nisiye na nguvu, nimeamua kukaa pembeni, siwezi kuingia ndani ya basi katika staili ya kusukumana au kupitia dirishani.
Kutokana na tabu ya usafiri, nalazimika kusubiri muda mrefu, huku pia nikitumia fursa hiyo kujifunza mengi kutoka kwa abiria wenzangu tunaosubiri usafiri kituoni hapo.
Kuna jambo naliona, linanivutia. Naamua kuelekeza umakini wangu kwenye jambo hilo. Ni mavazi hasa waliyovaa wanaume.
Napoteza muda na kuhesabu ‘kimya kimya’, moja, mbili, tatu, nne...nagundua wanaume wengi wamevaa suruali nyeusi. Katika 10, nabaini zaidi ya nusu rangi nyeusi ndiyo imetawala.
Kati ya idadi inayobaki, wamevaa suruali zenye rangi mbalimbali. Najisemea moyoni…haiwezekani, narudia kuhesabu kwa mara nyingine, majibu yaleyale.
Naendelea na utafiti wangu ofisini. Naangalia mavazi waliovaa wenzangu, suruali nyeusi kila kona. Kati ya watano, watatu suruali zao ni rangi nyeusi.
Kwa nini suruali nyeusi zimetawala?
Najiuliza, nataka kwenda mbali zaidi kujua sababu, nafikia uamuzi wa kuwauliza baadhi ya wanaume na wanawake siri ya rangi nyeusi.
Namuuliza George Ambindwile, mhadhiri Chuo Kikuu Dar es Salaam, ambaye mbali na kumfahamu ni miongoni mwa watu wanaopenda kuvaa suruali nyeusi.
Anasema wengi wanapenda suruali nyeusi kwa sababu, kwanza hazina gharama kuzinunua, lakini pia rangi zake hazikeri kama rangi nyingine.
Anaongeza: “Ni vigumu sana kumwona mwanaume amevaa suruali ya rangi nyekundu, kijani au nyingine yenye rangi inayoweza kumfanya kuonekana akiwa mbali.”
Ambindwile anasema kutokana na wanaume wengi kufanya kazi za nguvu kama kwenye gereji, viwandani na kazi zingine, suruali nyeusi huficha uchafu.
Kwa maelezo ya haraka haraka, alisema suruali nyeusi zinapendwa zaidi watu kwa sababu gharama yake ni nafuu.
Kwa upande wake, Zakaria Haule anasema yeye ni mpenzi wa kuvaa suruali nyeusi na sababu kubwa anaitaja ni suala la uchumi. “Suruali nyeusi hazina bei dukani, kwetu sisi walalahoi ndiyo kimbilio letu,” anasema na kuongeza:
Kwa upande wake, Dennis Osward msimamizi wa kituo cha kulea watoto yatima cha Mwanzo wa Nuru cha Victoria, anasema suruali nyeusi ndivyo vazi sahihi la walalahoi.
Anasema: “Suruali nyeusi haifuliwi mara kwa mara kwa sababu huficha uchafu tofauti na zingine. Kutofuliwa mara kwa mara, kunaifanya kudumu muda mrefu.”
“Unahitaji usafi kidogo unapokuwa na suruali nyeusi. Unaweza kuivaa zaidi ya mara tatu na kuendelea bila kuonekana kama ni chafu.”
Jannifer Sumi naye hakuwa mbali na mjadala wa suruali nyeusi. Anasema: “Wanaume wa kawaida siyo watu wa fasheni kama wanawake, hivyo hupenda nguo rahisi kama suruali nyeusi.
“Fasheni huendana na rangi kadhaa, wanaume wengi siyo wachaguaji wazuri wa rangi, lakini pia hawapendi rangi za kuwaonyesha kirahisi mbele ya macho ya watu.”
Vazi pekee rahisi kwao ni rangi nyeusi. Sumi anakubali kuwa kuna wanawake wengi pia hupenda rangi nyeusi, ingawa sababu zinaweza kuwa tofauti na zile za wanaume.
Kwa upande wake, Noor Shija anasema wanaume hupendeza zaidi wanapovaa suruali za rangi nyeusi kuliko rangi nyingine yoyote.
Anasema: “Suruali nyeusi zina faida kubwa kuliko kinyume chake. Kwanza, ndiyo rangi unayoweza kuvaa na shati lenye rangi yoyote.
Pia, mtu anapovaa suruali nyeusi, anaweza kufunga mkanda wa rangi yoyote. Kwa ufupi, rangi nyeusi ndiyo inayowafaa wanaume.”
“Ukiwa na suruali nyeusi, unaweza kuvaa na shati lenye rangi yoyote, liwe shati la bluu, jekundu, jeupe na hata njano.
Sabato Mwakipesile, anayemiliki ofisi ya ushonaji nguo ‘Pendeza Dress’ ya Mbezi Luis, anakiri wanaume wengi kupenda kuvaa suruali nyeusi, akiwamo yeye mwenyewe.
Anasema katika ofisi yake, kati ya suruali 10 anazoshona kila wiki, sita huwa na rangi nyeusi na zinazobaki huwa na rangi tofauti, lakini zinazokaribiana na nyeusi kama ‘Dark Blue’.
Anasema: “Mbali na kushona, pia nauza vitambaa mbalimbali, lakini vile nyenye rangi nyeusi ndiyo vinapendwa zaidi na wateja wanawake kwa wanaume.”
Kuhusu kwa nini wanaume wanapenda suruali nyeusi, anasema: “Ni vazi rahisi, halichakai mapema, ni rahisi kuficha uchafu, bei yake siyo kubwa na likishonwa vizuri linapendeza mwilini.”
Kwa upande wake, Jumanne Mussa mkazi wa Kijitonyama, anasema wanaume wanapende suruali nyeusi kwa sababu ndiyo tafsiri ya kupendeza kwa mwanaume.
Anasema: “Angalia viongozi au watu maarufu duniani, vazi lao kubwa ni suti nyeusi. Hata kwenye sherehe za harusi, bwana harusi hupendeza zaidi akiwa na suti nyeusi kuliko rangi nyingine.”
Kwa upande wake, Lilian Timbuka anasema sababu kubwa ya wanaume kupenda suruali nyeusi ni kwa sababu ya ‘upofu’ katika kuchagua rangi.
“Wanaume siyo wachaguaji wazuri wa rangi, lakini pia hawana mvuto na rangi kali au za kumeremeta. Macho yao ni mepesi kuona rangi kali, lakini hawapendi rangi za aina hiyo,” anasema.
MAKALA KUTOKA GAZETI LA MWANANCHI.... Joseph Kapinga

Tags:

Share This Post

Get Updates

Subscribe to our Mailing List. We'll never share your Email address.

0 comments:

ddsdfs


Powered by Blogger.
back to top