Dar es Salaam. Waziri wa Uchukuzi Samuel Sitta
amemsimamisha kazi Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania
(TPA), Madeni Kipande baada ya kuwepo malalamiko ya ubabaishaji katika
zabuni mbalimbali za mamlaka hiyo.
Hatua hiyo ya Sitta imekuja wiki tatu baada ya
kuteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuiongoza wizara hiyo akitokea
Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kabla, wizara hiyo ilikuwa chini ya Dk
Harrison Mwakyembe.
Sitta, ambaye pia hujulikana kama Mzee wa Viwango,
amewaambia waandishi wa habari jijini hapa leo kuwa wadau mbalimbali
wamesema taratibu za zabuni TPA haziendeshwi kwa uwazi na uaminifu.
“Wanasema hakuna uwazi katika zabuni, kuna dalili
ya ubabaishaji. Katika kamati za kutathmini zabuni majina ya watu
yanabadilika badilika na hata baada ya mshindi kupatikana bodi huchelewa
kutoa barua inayohusu uamuzi wa kumpata mshindi huyo,” amesema Sitta.
“Hayo yote yanajenga taswira isiyo nzuri kwa bandari, serikali na nchi nzima kwa ujumla,”
Kwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji ndiye msimamizi mkuu
wa shughuli za bandari, amesema ameamua kumsimamisha Kipande kupisha
uchunguzi kwa kipindi hicho na nafasi yake itachukuliwa na Meneja
Bandari ya Dar es Salaam, Awadh Massawe.
Kutokana na kusimamishwa kwa kigogo huyo, Sitta
aliitangaza tume maalumu ya watu sita itakayochunguza tuhuma hizo
ikiongozwa na Jaji Mstaafu Augusta Bubeshi na itafanya kazi hiyo kwa
majuma mawili.
Wengine katika tume hiyo ni Mkurugenzi Mkuu
Mstaafu wa Mamlaka ya Manunuzi ya Umma (PPRA) Dk Ramadhan Mlinga,
Mkurugenzi Mkuu Mstaafu wa TPA Samson Luhigo, aliyekuwa Naibu Mkurugenzi
Mkuu, TPA Happiness Senkoro.
Pia, katika tume wapo Mkurugenzi wa Masoko mstaafu
wa TPA Flavian Kinunda na Mtumishi wa Wizara ya uchukuzi Deogratius
Kassinda atakaye kuwa Katibu.
“Nimejitahidi kuwachukua hawa wastaafu kwa kuwa
kwa sasa hawatafuti cheo chochote na tunaamini watatenda haki kwa
kuchunguza tu bila uonevu wowote.
“Ni muhimu sana taratibu za bandari ziwe wazi,
ziheshimike duniani kote kwa kuwa miradi ya bandari ni mikubwa sana
inayopitishwa na bodi ya zabuni ya bandari,” amesema Sitta
Hata hivyo Waziri Sitta baada ya kumaliza
kuzungumza na waandishi hakutaka kuruhusiwa kwa swali lolote kwa madai
kuwa anamajukumu mengine.
0 comments: